“SIKU YA WAJINGA” (AprilFool) ni Kielelezo cha kufilisika Ubepari Kimaadili.
Ni jambo la kawaida ndani ya mfumo wa kibepari kukuzwa mambo ya kipuuzi na yasiyo na msingi kwa kupewa kipaumbele na kutangazwa katika vyombo vya habari vya kitaifa na kimataifa.
Miongoni mwa mambo maarufu ya kipuuzi yanayopewa nafasi kubwa katika jamii ni ile siku inayoitwa ‘siku ya wajinga duniani ‘ April fool’s day. Ndani ya siku hii ya mwanzo ya mwezi wa Aprili katika kila mwaka watu, taasisi, mashirika na vyombo vya habari mbali mbali hutoa taarifa za uongo bila ya kujali madhara au usumbufu utakaojitokeza kwa kisingizio cha Siku ya wajinga duniani.
Aidha, fedha na muda mwingi kupotea kwa mambo kama haya ambapo fedha hizo na muda ungeweza kutumika kukabiliana na matatizo mengi yanayowakumba wanadamu kama njaa, maradhi, ukosefu wa maji safi, makaazi n.k.
Allah Taala amekemea suala hili pale Aliposema:
بَلْ هُمْ فِي شَكٍّ يَلْعَبُونَ (الدخان: 9).
“Bali wao wapo katika pumbao lao wanacheza” (TMQ Ad-Dukhan : 9)
Miongoni mwa maelezo yanayotolewa kuhusiana na historia ya siku hiii ya Apri Fool ni kauli ya Profesa wa Historia Joseph Boskin wa Chuo kikuu cha Boston Marekani, ambae anadai kuwa chanzo cha siku hii ni kipindi cha utawala wa Constantine ndani ya Roma (305). Alipofuatwa mfalme huyo na wanasarakasi na wajinga kumuomba awape nafasi ya kuendesha shughuli za kiutawala angalau kwa siku moja. Mwanasarakasi mmoja kwa jina Kugel alipewa nafasi hiyo ya kuwa mfalme kwa siku moja na akapitisha kanuni ya kufanya mambo mengi ya kipuuzi ndani ya siku hiyo. Na tamaduni hii ikakita mizizi tokea kipindi hicho. http://www.infoplease.com/spot/aprilfools1.html.
Tabia hii imeota na kuchukua nafasi kubwa katika jamii hata za Waislamu kiasi cha kujiona kwamba wako huru na hawapati madhambi lau watajihusisha katika upuuzi na kudanganya ndani ya siku hii.
Mkazi mmoja wa maeneo ya Mikanjuni mkoani Tanga alipigwa faini ya shilingi laki tano miaka mitatu iliyopita kwa sababu ya kutoa taarifa ya uongo ya kutokea moto katika eneo lake, baada ya kupokea simu hiyo magari kadhaa ya zima moto yalielekea katika eneo waliloelekezwa na mpiga simu lakini cha ajabu walipofika katika eneo hilo walitafuta tafuta sehemu yote bila kukuta ishara yoyote ya moto. Ni baada ya kushirikiana na mitandao ya simu ndipo walipofanikiwa kumkamata muhusika na akafikishwa mahakamani. www.jamiiforums.com/…na…/426538-1st-april-fools-day-2013-tahadhari-leo-ni-siku-ya-wajinga-kuweni-makini.html
Hili ni katika baadhi tu ya matukio mengi ambayo yamewakumba, kuwapotezea muda na kuwadhuru watu wengi. Pia baadhi ya vyombo vya habari na magazeti hushadidia taarifa za uwongo wa kiudhuru kama kutangaza nafasi za ajira, kutolewa kwa misaada nk. Matokeo yake watu wazima, vikongwe na madhaifu hukusanyika kutaraji misaada hiyo na mwishowe kuishia patupu eti kwa kigezo tu cha ‘april fool’.
Ndani ya Uislamu, uwongo umekatazwa na ni haramu ila katika hali maalum. Na mambo hayo hayapewi nafasi kabisa katika jamii ya Kiislamu. Na uwongo katika kiwango cha kumdhuru mwengine mahkama ya kadhi hutoa adhabu kali ya taazir kwa mtendaji. Na adhabu ya Akhera ni kubwa zaidi. Bila ya kusahau kwamba itikadi ya Uislamu imefunga kwamba vitendo vyote vya mwanadamu ndani ya dunia hii kufungamanishwa na maisha yajayo ya akhera. Ikiwa na maana kuwa vyote vitahesabiwa. Kama ni vitendo vyema mtendaji atastahiki ujira mzuri na kama ni viovu mtendaji atastahiki adhabu.
فَمَنْ يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ خَيْرًا يَرَه: وَمَنْ يَعْمَلْ مِثْقَالَ ذَرَّةٍ شَرًّا يَرَه (الزلزلة: 7
“Basi anayetenda wema mithili ya tembe atauona! Na anayetenda uovu mithili ya tembe atauwona!”(TMQ 99: 7-8)
Muhija Zubeir